11/04/2019
SERIKALI ya nchini Sudan, leo imeondolewa madarakani na jeshi la ulinzi la nchi hiyo, na kutangaza kumk**ata Rais Omar Al-Bashir.
Kiongozi huyo ambaye amekaa madarakani kwa miaka 30, ameondolewa kufuatia maandamano ya wananchi ambayo yamedumu kwa takribani miezi kadhaa.
Kwa mujibu wa taarifa ya kijeshi iliyosomwa kwenye televisheni ya taifa nchini humo leo Alhamisi Aprili 11, 2019, imesema Al Bashir amevuliwa kwa nguvu cheo cha kuwa kiongozi mkuu na kupelekwa "sehemu salama."
Akitoa taarifa kwa umma ya kuondolewa kiongozi huyo, Makamu wa Bashir ambaye pia ni Waziri wa Ulinzi wa Sudan, Jenerali Awad Ibn Auf, amesema kuanzia sasa nchi hiyo itaongozwa na serikali ya mpito ya kijeshi itakayotawala kwa miaka 2.
"Jeshi la ulinzi limechukua madaraka ya kuongoza wananchi ili kurejesha utengamano kwa Wasudan wote kuishi kwa amani na utulivu," imesema taarifa hiyo na kukaririwa na shirika la habari la Ufaransa (AFP).
Jenerali Auf ametangaza hali ya hatari ya miezi 3 sanjari na kusimamisha Katiba ya nchi hiyo, ambayo ilitungwa mwaka 2005.
Jenerali huyo amesema kuwa anga ya nchi hiyo imefungwa kwa saa 24 zijazo kuanzia tangazo hilo, na pia kufungwa mipaka yote ya Sudan.
Akitangaza vipaumbele vya serikali hiyo mpya, jenerali huyo amesema taasisi zote za kiutawala nchini humo, likiwemo bunge na baraza la mawaziri zimevunjwa ili kutoa nafasi ya kile alichokiita ni "kutoa nafasi ya kuandaliwa uchaguzi mkuu huru na wa haki.
Omar Bashir (75) ambaye pia ni Jenerali wa jeshi alishika madaraka ya kuongoza Sudan akiwa Rais wa 7 mwaka 1989, kufuatia mapinduzi yaliyoondoa serikali ya kiraia ya Waziri Mkuu Sadiq Al-Mahdi (sasa umri miaka 83).
Al Bashir ambaye licha ya kuwa na wake 2 hana mtoto, mwaka 2008 alikabiliwa na shinikizo la kimataifa kutaka ak**atwe na kupelekwa kwenye mahak**a ya kimataifa ya jinai (ICC), yenye makao makuu mjini The Hague nchini Uholanzi.
Serikali yake ilikuwa ikishutumiwa kwa tuhuma za mauaji ya wananchi wa jimbo la Darful nchini humo, katika vita ya wenyewe kwa wenyewe.